Genesis 32

Yakobo Ajiandaa Kukutana Na Esau

1Yakobo pia akaondoka akaenda zake, nao malaika wa Mungu wakakutana naye. 2Yakobo alipowaona, akasema, “Hii ni kambi ya Mungu!” Kwa hiyo akapaita mahali pale Mahanaimu.
Mahanaimu maana yake Kambi mbili.

3Yakobo akatuma wajumbe kumtangulia kwa Esau ndugu yake huko Seiri, katika nchi ya Edomu. 4Akawaagiza akisema: “Hili ndilo mtakalomwambia bwana wangu Esau: ‘Mtumishi wako Yakobo anasema, nimekuwa nikiishi pamoja na Labani na nimekuwako huko mpaka sasa. 5Ninao ng’ombe na punda, kondoo na mbuzi, watumishi wa kiume na wa kike. Sasa ninatuma ujumbe huu kwa bwana wangu, ili nipate kibali machoni pako.’ ”

6Wajumbe waliporudi kwa Yakobo, wakamwambia, “Tulikwenda kuonana na ndugu yako Esau, naye sasa anakuja kukulaki akifuatana na wanaume 400.”

7Kwa hofu kuu na huzuni, Yakobo akagawanya watu aliokuwa nao katika makundi mawili, pia akagawanya makundi ya kondoo na mbuzi, na vilevile ng’ombe na ngamia. 8Yakobo alifikiri, “Kama Esau akija na kushambulia kundi moja, kundi lililobaki litaweza likanusurika.”

9Ndipo Yakobo akaomba, “Ee Mungu wa baba yangu Ibrahimu, Mungu wa baba yangu Isaka, Ee Bwana, ambaye uliniambia, ‘Rudi katika nchi yako na jamaa yako, nami nitakufanya ustawi,’ 10mimi sistahili fadhili na uaminifu wako wote ulionitendea mimi mtumishi wako. Nilikuwa na fimbo tu mkononi mwangu nilipovuka mto huu wa Yordani, lakini sasa ninayo makundi mawili. 11Nakuomba, uniokoe na mkono wa ndugu yangu Esau, kwa maana ninaogopa kuwa atakuja kunishambulia, pia mama pamoja na watoto wao. 12Lakini umeshasema, ‘Hakika nitakufanya ustawi na kuufanya uzao wako kuwa mwingi kama mchanga wa baharini ambao hauwezi kuhesabika!’ ”

13Akalala pale usiku ule, miongoni mwa vitu alivyokuwa navyo, akachagua zawadi kwa ajili ya Esau ndugu yake: 14Mbuzi waume ishirini na mbuzi wake 200, kondoo dume ishirini na kondoo wake 200. 15Ngamia wake thelathini pamoja na ndama zao, ng’ombe wake arobaini na mafahali kumi, punda wake ishirini na punda waume kumi. 16Akaviweka chini ya uangalizi wa watumishi wake, kila kundi peke yake na kuwaambia, “Nitangulieni na kuacha nafasi kati ya makundi.”

17Akamwagiza yule aliyetangulia kuwa, “Ndugu yangu Esau atakapokutana nawe na kukuuliza, ‘Wewe ni wa nani? Unakwenda wapi? Wanyama hawa wote mbele yako ni mali ya nani?’ 18Ndipo utakaposema, ‘Ni mali ya mtumishi wako Yakobo. Ni zawadi ambazo zimetumwa kwa bwana wangu Esau, naye anakuja nyuma yetu.’ ”

19Akamwagiza pia yule mtumishi wa kundi la pili, la tatu na yale mengine yote yaliyofuata akiwaambia, “Mtamwambia Esau maneno hayo hayo mtakapokutana naye. 20Hakikisheni mmesema, ‘Mtumishi wako Yakobo anakuja nyuma yetu.’ ” Kwa kuwa alifikiri, “Nitaweza kumtuliza kwa zawadi hizi ninazotanguliza, hatimaye, nitakapomwona, huenda atanikubali.” 21Kwa hiyo zawadi za Yakobo zilitangulia mbele yake, lakini yeye mwenyewe alilala kambini usiku ule.

Yakobo Ashindana Mweleka Na Mungu

22Usiku ule Yakobo akaamka akawachukua wake zake wawili, watumishi wake wawili wa kike na wanawe kumi na mmoja na akavuka kivuko cha Yaboki. 23Baada ya kuwavusha ng’ambo ya kijito, alivusha pia mali zake zote. 24Kwa hiyo Yakobo akaachwa peke yake na mtu mmoja akashikana naye mweleka mpaka mapambazuko. 25Yule mtu alipoona kuwa hawezi kumshinda, aligusa kiungio cha nyonga ya Yakobo kwa hiyo nyonga yake ikateguka wakati alipokuwa akishikana mweleka na yule mtu. 26Ndipo yule mtu akasema, “Niache niende, kwa kuwa ni mapambazuko.”

Lakini Yakobo akajibu, “Sitakuacha uende usiponibariki.”

27Yule mtu akamuuliza, “Jina lako nani?”

Akajibu, “Yakobo.”

28Ndipo yule mtu akasema, “Jina lako halitakuwa tena Yakobo, bali Israeli,
Israeli maana yake Yeye ashindanaye na Mungu.
kwa sababu umeshindana na Mungu na watu pia, nawe umeshinda.”

29Yakobo akasema, “Tafadhali niambie jina lako.”

Lakini akajibu, “Kwa nini kuniuliza Jina langu?” Ndipo akambariki huko.

30Kwa hiyo Yakobo akapaita mahali pale Penieli,
Penieli maana yake Uso wa Mungu, ambalo ni sawa na Penueli kwa Kiebrania.
akasema, “Ni kwa sababu nimemwona Mungu uso kwa uso na bado maisha yangu yameokoka.”

31Jua lilikuwa linachomoza Yakobo alipoondoka Penueli, naye alikuwa akichechemea kwa sababu ya nyonga yake. 32Kwa hiyo mpaka leo Waisraeli hawali mshipa ulioungana na kiungio cha nyonga, kwa sababu kiungio cha nyonga ya Yakobo kiliteguliwa karibu na mshipa huo.
Copyright information for SwhKC